HABARI MPYA

6/recent/ticker-posts

Mkutano wa kwanza Zanzibar, mabadiliko tabianchi

 


TAMWA ZNZ , Kitengo cha habari

Chama cha waandishi wa habari Wanawake Tanzania, TAMWA ZNZ kwa kushirikiana na wadau wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ikiwemo Taasisi ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (ZACCA) na Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais Zanzibar, imeandaa mkutano wa kwanza wa mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika  Zanzibar, oktoba 20 hadi 22 katika Ukumbi wa Idrissa Abdulwakil.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za TAMWA Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja, Mwenyekiti wa kamati ya Jukwaa la mabadiliko ya tabianchi Zanzibar.(ZANCCC) Mahfudh Shaban Haji, amesema lengo la mkutano huo ni kujenga uwezo, uelewa na hamasa kwa asasi za kiraia, wanajamii na Idara za Serikali kufahamu dhana nzima ya mabadilikoya tabianchi na uhimili wake.

 Aidha Shaaban ameeleza kuwa mkutano huo utazungumzia mada mbali mbali za kimataifa na kitaifa ikiwemo mkakati wa mabadiliko ya tabianchi wa mwaka 2014, sera, uwajibikaji na dira ya maendeleo 2050 ambayo inakwenda sambamba na mipango ya kimataifa ya maendeleo endelevu ya SDGs.

 

 

‘’Mabadiliko ya Tabianchi ni suala mtambuka hivyo tutajenga uelewa juu ya mchango wa asasi za kiraia, kuimarisha usimamizi na utekelezaji wa uhifadhi na uhimili wa mabadiliko ya tabianchi,” Mahfoudh.

Nae Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wahabari Wanawake Tanzania, TAMWA ZNZ Dkt Mzuri Issa amewataka waandishi wa habari kuandika habari zinazoibua changamoto za mabadiliko ya tabianchi ili ziweze kuwafikia walengwa na kufanyiwa kazi.

 ‘’waandishi wahabari tumieni kalamu zenu kuyaibua na kuyafanyia uchechemuzi masuala ya mabadiliko ya tabianchi kwa upana wake’’ Dkt Mzuri Issa TAMWA ZNZ.

Kwa upande wake mwakilishi wa Taasisi ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ZACCA Ngwali O. Ngwali amesema Ukataji wa mikoko unachochea zaidi Mabadiliko ya tabia nchi katika maeneo ya fukwe za bahari ambapo katika maeneo ya Mkokotoni,fungurefu na Donge kwa Mkoa wa Kaskazini Unguja, yameathirika kwa kiasi kikubwa.

Aidha amewaomba wanajamii kuyalinda mazingira ili kuirithisha Zanzibar ya kijani kwa lengo la kuepuka athari zinazoendelea kujitokeza.

Jumla ya washiriki 250 kutoka ndani na nje ya Zanzibar watashiriki mkutano huo, unaotarajiwa kufunguliwa na Waziri wa Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mh Harusi Said Suleiman na kauli mbiu ni “ imarisha uhimili wa mabadiliko ya tabianchi Zanzibar “

Mwisho

Post a Comment

0 Comments