HABARI MPYA

6/recent/ticker-posts

Wataalam wa Kilimo Pemba wahimizwa uwajibikaji kwenye utekelezaji mradi wa VIUNGO

Washiriki wakiendelea na mafunzo

Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Said Yussuf Kombo akiendesha mafunzo

Washiriki baada ya kukabidhiwa vyeti

KATIBU tawala wilaya ndogo ya Kojani Makame Khamis Makame, akizungumza na washiriki wakati wa ufungaji wa mafunzo.

KATIBU tawala wilaya ndogo ya Kojani Makame Khamis Makame, akimkabidhi cheti cha ushiriki wa mafunzo mmoja wa washiriki wa mafunzo.

Washiriki wakiwa wameshakabidhiwa vyeti vyao.

Na Mwandishi wetu. 

KATIBU tawala wilaya ndogo ya Kojani Makame Khamis Makame, amewataka mabini na mabwana shamba waliopatiwa mafunzo maalum ya taaluma juu ya namna ya uendeshaji wa shama darasa kupitia mradi wa Viungo kuhakikisha wanafikisha elimu kwa wakulima wote waliotayari kujishughulisha na shughuli hizo ili kuweza kufanikisha malengo ya mradi huo kwa wakulima.

Akizungumza katika hafra ya kufunga mafunzo ya siku tano kwa wataalam wa kilimo 42 kutoka kwenye Shehia zote za Pemba ambazo mradi huo unatekelezwa, katibu huyo amesema ili kufikia malengo ya kuwainua wakulima kiuchumi ni lazima kuwa waangalifu wakati wa kuchagua wakulima wa kusaidiwa kupitia mradi huo.

Alisema mradi huo kupitia mpango wake wa utoaji wa elimu ya shamba darasa kwa wakulima itawasaidia kuondokana na uzalishaji wa mazoea na badala yake kuzalisha mazao kwa kutumia zana za kisasa na hatimaye kuongeza tija kwa kuzalisha mazao bora na kwa wingi.

“Tunapokwenda kwenye utekelezaji, twende na watu ambao wapo tayari. Si kwa misingi kwamba huyu ni mtoto wa bwana shamba, hatutaki. Tunataka wakulima ambao wamejitoa wenyewe kwa ridhaa zao kwamba ni wakulima ili tuone kwamba mradi huu kweli mwisho wa siku unaleta tija kwa wakulima wetu kuongeza vipato vyao,” alisema.

Aidha alisema Serikali za Wilaya na Mkoa zitaendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu katika ngazi ya shehia ili kujiridhisha na utekelezaji wa mradi huo kwa wakulima kwa lengo la kusaidia ufanisi na utekelezaji wa malengo ya mradi huo.

Alisema, “kwa niaba ya ofisi ya mkuu wa Wilaya  kupitia wizara ambayo ni mdau ya Tawala za mikoa, katika hili naahidi kwamba tutakuwa pamoja huko kwenye saiti kuanzia masheha wetu,  lazima tupite kukagua kuona kama shughuli zinaenda kama zilivyopangwa kwani wakulima nao muda mwingine wanakuwa wababaishaji.”

Aliongeza, “Wananchi wetu wamezoea kuona miradi mingi inakuwa hai pae inapokuwa katika kipindi cha utekelezaji na inapomaliza muda wake wanarudi nyuma. Hili hatutaki lijitokeze katika mradi huu wa viungo.”

Mapema meneja wa mradi huo, Sharif Maalim Hamad alisema mafunzo hayo yametolewa kwa lengo la kuwapatia taaluma juu ya namna ya uendeshaji wa shamba darasa ili kurahisisha ufikiaji wa lengo la mradi kwa kuwafikia wakulima 10,500 kwa upande wa Pemba.

Alisema kutokana na mradi kuhitaji kufikia idadi kubwa ya wakulima katika utekelezaji wake, wataalamu hao watatumia mbinu walizofundishwa kuwafikia wakulima hao kupitia mfumo wa shamba darasa ili matokeo yaweze kupatikana kwa haraka zaidi.

“Mafunzo haya lengo letu kubwa ni kuwapa taaluma juu ya namna ya uendeshaji wa skuli za wakulima. Kwasababu shughuli za wakulima ndio kitu muhimu katika utekelezaji wa mradi huu, wataalam wa CFP pekee yao hawataweza kuwafikia wakulima 21,000 kwa unguja na pemba kwa hivyo tukaona tuwashirikishe hawa ili tugawiane maeneo ili lengo la mradi lifanikiwe,” alisema.

Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Said Yussuf Kombo alibainisha kuwa katika mafunzo hayo mada mbalimbali zimefundishwa ikwa ni pamoja na dhana ya shamba darasa pamoja na mbinu za Uchunguzi wa mazao shambani (UMASHA).

Alisema, “wataalamu hawa tumewakumbusha zaidi kuhusu misingi ya utoaji wa elimu kwa wakulima kupitia shamba darasa ambapo pia wameweza kujifunza kwa vitendo mbinu za uchunguzi wa mazao shambani (UMASHA) lengo likiwa ni kuwasaidia wakulima kufanya tafiti ndogondogo za mazao yao.”

Mshiriki wa mafunzo, Sabra Hamad Ali alisema kutolewa kwa mafunzo hayo yatawawezesha kufikisha elimu kwa wakulima katika njia ambayo ni rahisi na kwa wakati kutokana na sahihi kulingana na mazingira ya wakulima wenyewe.

“Tunashukuru sasa tumepata taaluma mpya na mbinu zaidi za kwenda kuwafundisha wakulima wetu kupitia shamba darasa, sasa tunakwenda kufanya kazi,” alisema.

Katika mafunzo hayo washiriki walibidhiwa hati za vyeti vya ushiriki ikiwa ni miongoni mwa hatua za kutambua ushiriki wao kikamilifu na utayari wa kuanza kutekeleza majukumu yao ili kufanikisha malengo ya mradi.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa  viungo, mboga na matunda unaotekelezwa Zanzibar na taaasisi za People’s Development Forum (PDF), Community Forests Pemba (CFP) na Chama cha Waandishi wa Habari wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA Zanzibar)  kupitia ufadhili wa Umoja wa Ulaya.


Post a Comment

0 Comments