HABARI MPYA

6/recent/ticker-posts

"AGRI-CONNECT Imesaidia Serikali kupunguza Umasikini kwa Wananchi Zanzibar" - Katibu Mkuu Kilimo


Na Mwandishi wetu

TAASISI zinazotekeleza miradi ya kilimo Zanzibar chini ya mpango wa AGRICONNECT Tanzania unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) zimetakiwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa shughuli za miradi ili kuchochea ufikiaji wa malengo ya kukuza mnyororo wa thamani kawenye mazao ya Viungo, Mboga na matunda nchini.

Ushauri huo umetolewa kufuatia ziara ya maafisa wa Wizara ya kilimo na ujumbe kutoka Umoja wa Ulaya iliyofanyika hivi karibuni Unguja na Pemba kutembelea wanufaika wa miradi hiyo kufanya tathimini ya maendeleo ya utekelezaji miradi hiyo.

Katibu mkuu Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar, Seif Shaban alipongeza juhudi zinazofanywa na program ya AGRICONNECT kuinua sekta ya kilimo Zanzibar na kusema utekelezaji wake umeanza kuzaa matokeo chanya kwa wakulima kuzalisha kwa kufuata mbinu bora za kilimo.

Aliongeza kupitia miradi hiyo ambayo inakuza uchumi wa wananchi, inaisaidia serikali kufikia lengo lake la kupunguza umasikini kwa wananchi wake na kuongeza fursa za ajira kwa vijana kupitia shughuli za kilimo.

Alieleza serikali kupitia wizara ya kilimo itaendelea kushirikiana na wadau wa miradi hiyo ili kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinatatuliwa kwa wakati na wakulima wanapata fursa ya kuzalisha kwa wingi mazao bila kikwazo na kukuza uchumi wao na taifa.

Kwa upande wake afisa kutoka Umoja wa Ulaya, Anna Constantini, alishauri mradi kushirikiana na wakulima kufanyia kazi upatikanaji wa mfumo wa kisasa wa masoko ili kuwawezesha wakulima kupata taarifa za masoko kwa njia ya kidijitali.

Amesema mfumo huo ukianza kufanya kazi utawasaidia wakulima kujua bei za mazao sokoni kupitia simu zao na kuondokana na uuzaji wa bidhaa kwa bei ya hasara kutokana na kukosekana kwa taarifa sahihi za masoko.

“Lazima mfumo wa masoko ufanye kazi ili kuwawezesha wakulima kujua nani wa kumuuzia bidhaa zao na wauze kwa bei nzuri ili kujikwamua kiuchumi,” alieleza Anna Costantini, afisa kutoka Umoja wa Ulaya (EU).

Mapema, Pili Kashinje Ali, mkulima kiongozi na msarifu wa mazao ya Viungo katika Shehia ya Mahonda, ambaye ni mnufaika wa mradi wa VIUNGO alishukuru uwepo wa mradi huo na kueleza kuwa umesaidia kurejesha matumaini ya wakulima kuwekeza katika kilimo.

Alisema, "mwanzo tulikuwa na changamoto ya kukosa mashine maalumu ya kusaga Viungo, lakini mradi tayari umetuletea mashine hiyo ambayo sasa inakwenda kuturahisishia kazi na kutuwezesha kuziongezea thamani zaidi bidhaa zetu ili kupata soko la uhakika kuliko kuuza kama mazao ya kawaida jambo ambalo linapelekea kuuza kwa bei ya hasara.

Nae Yasin Swalehe Kuhaka, miongoni mwa vijana walionufaika na utekelezaji wa mradi huo alieleza uwepo wa mradi wa ACRICONNECT umehamasisha vijana kuona fursa ya kujiingiza katika kilimo na kuondokana na dhana mbaya kuhusu shughuli za kilimo.

Anaeleza, "baada ya kuhitimu elimu yangu ya chuo nilikuwa sina mwelekeo kama kijana, lakini kutokana na kukaa mtaani bila kazi niliamua kuingia katika kilimo baada ya kuhamasishwa na kiongozi wangu Pili Kashinje ambaye ni mzoefu katika kilimo alinishika mkono na kunielekeza kila hatua, na nashukuru baadae nilipata fursa ya kufikiwa na mradi huu wa AGRICONNECT ambao umenisaidia kuona thamani ya kilimo."

Katika ziara hiyo, wanufaika wa mradi wa VIUNGO unaotekelezwa kwa Mashirikiano na People’s Development Forum,(PDF), Community Forests Pemba (CFP), na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ) walitembelewa na kuainisha changamoto zinazowakabili wakulima hao.

Post a Comment

1 Comments