HABARI MPYA

6/recent/ticker-posts

JAMILA BORAFYA HAMZA: KIONGOZI MWENYE UWEZO, AKILI NA MAARIFA

 


Na Raiffa Abdallah

Wataalamu wa sayansi ya jamii wanaamini kwamba uongozi ni rasilimali muhimu ya kuchangiza maendeleo ya jamii na ndiyo sababu nchi za kidemokrasia zinafanya uchaguzi kila baada ya miaka fulani ili kupata  viongozi bora. 

Katika miaka ya nyuma ilikuwa  siyo rahisi  kukuta mtu mwenye ulemavu  anapewa fursa ya kuwa kiongozi. Lakini baada ya kuanza kupewa jukumu hilo wapo waliothibitisha kwamba  wana uwezo mkubwa wa kiuongozi.

 Jamila Borafya Hamza  anayeishi Mwanakwerekwe Zanzibar ni mmoja wa watu wenye ulemavu wa macho, lakini kwa jinsi alivyoshika nafasi nyingi za uongozi  na anavyopambania  maslahi ya watu wewe siyo rahisi ukatambua kwamba ana ulemavu huo.

"Kilichonivutia zaidi kuingia kwenye uongozi nilikuwa natamani watu waone watu wenye ulemavu tunaweza kuongoza”, amesema Jamila ambaye ni Mjumbe Baraza la Watendaji Taifa katika Baraza la Vijana Zanzibar  na kuongeza;.

 ‘’Nilikuwa najiamini na kuamini naweza  na  familia ilikuwa inanitia moyo nikawa nazidi kuhisi naweza na kweli  nikawa naweza kuongea mbele za watu, nasafiri sehemu mbali mbali na kutatua kero za watu."

Binadamu bila kujali ana ulemavu au la, hakuna ambaye anaweza kutekeleza majukumu yake yote bila kutegemea watu wengine.

Jamila anasema, anatekeleza majukumu yake ya kiuongozi kutokana na msaaada anaoupata kwa watu  anaofanya nao kazi .

Lakini anasisitiza "hata mimi mwenyewe sijajiweka nyuma ,maana natafuta mtu wa kufatana nae maana sheria zinatutaka tutembee na wasindikizaji, na mimi huwa natekeleza majukumu yangu hata kama hawajaniwezesha kikamilifu na mwisho hawamini wanachokiona".

 

MAMBO KUJIVUNIA ALIYOWAFANYIA ANAOWANGOZA

Watu wenye busara husikika wakisema uongozi ni kuacha alama nzuri kwa wale uliowaongoza au unaoendelea kuwaongoza.

Kuna vitu vingi Jamila amevifanya mpaka sasa kwa vijana anaowaongoza  na vimeweka alama katika mioyo ya vijana hao.

"Kiongozi Jamila anafanya mambo makubwa sana ambayo muda mwingine ni vigumu mtu mwenye hali kama yake kufanya maana, anakwenda masafa marefu kuhudhuria vikao bila ya kujali hali yake, tunamuamini na vijana wengi sana na tunamsikiliza", amesema Fatawi Habib Khamis mwanachama Baraza la vijana.

Mjumbe mwingine wa baraza hilo  Zainab Mtumwa Ame, anasema "Jamila anafanya kazi zake za uongozi katika mazingira magumu lakini matokeo yake anachofanya ni mazuri na hutengemei , yuko mbele kwa kila kitu na anajiamini kueleza shida za vijana hata awe nani anasema na mwisho wa mazungumzo yake lazima aeleze nini kifanyike ili kutatuwa tatizo alilowasilisha".

Jamila  anasema yeye anamini mambo mengi sana mazuri huwafanyia watu wanaowaongoza ambayo mpaka sasa yamewacha alama kwenye maisha yao.

Anasema " vijana wengi kupitia mimi wamepata ajira kwa kuajiriwa au kujiajiri na hii ni kutokana na miongozo yangu ninayowapa vijana ninao waongoza na mpaka sasa wengi wao wananishukuru maana nimewafundisha ujasiri mkubwa sana ".

Pia amesema kuwa wapo vijana kupitia muongozo wake wamepata fursa nje ya Zanzibar.

CHANGAMOTO KATIKA UONGOZI WAKE

 Kila kazi inachangamoto yake katika utekelezaji na ndo ilivyo pia kwa Jamila Borafya Hamza. Katika maisha ya uongozi wake licha ya kutekeleza majukumu yake kwa uweledi mkubwa  anapitia changamoto nyingi sana.

Hata hivyo yeye binafsi haoni ni changamoto, bali  anachukuliya hizo changamoto kama ni fursa kwake.

 "Changamoto kubwa ni ulemavu wa macho, ninapotaka kugombea mtu haniamini anaona yule ataongozaje lakini anasahau kwamba macho siyo yanayongoza isipokuwa akili na maarifa", amesema Jamila

Vile vile Jamila ametaja changamoto ya mazingira anayofanyia kazi sio rafiki na hivyo hupelekea ugumu katika utekelezaji wa majukumu yake , akataja rasilimali fedha kuwa pia ni miongoni mwa changamoto.

Kadhalika amesema ingawa anapambana  hana vifaa saidizi ndiyo maana baadhi ya maeneo ushiriki wake unakuwa mdogo.

  ANAVYOTATUA CHANGAMOTO

Mshairi moja aliwahi kusema  "mwenye mapenzi haoni ingawa anayomacho". Changamoto hizo Jamila kwake haoni kama ni kikwazo cha kwamba yeye asitekeleze majukumu yake. Badala yake  anazitatua changamoto hizi kwa kujiamini na kupambana kwa kila hali.

"Ukiwa kiongozi na ukiwa unajiamini lazima uwe na ushawishi mzuri kwa vijana au kwa wale unaowaongoza”, anasema Jamila na kuongeza:

“Maana wale ninaowaongoza ushawishi wangu na utamu wa maneno yangu wanakuwa wanakubali na pia tunatatuwa changamoto hizi kwa kupambana na kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi zaidi’’.

MAZUNGUMZO NA BABA YAKE

Jamila ni kijana anayeishi na wazazi wake wote wawili baba na mama. Mwandishi wa makala hii ameamuwa kukaa chini na baba mzazi wa Jamila na kutaka kujuwa mengi kuhusu mtoto wake, tangu utoto wake mpaka kukua na haswa katika uongozi.

Baba mzazi wa Jamila  mzee Borafya Hamza amesema Jamila alizaliwa akiwa na ulemavu wa macho lakini uwezo wake wa kuongoza.

“Sisi wazazi  tulianza  kuona uhodari wake tangu akiwa mtoto mdogo sana maana alipokuwa akicheza na watoto wenziwe alipenda kuigiza kama mama, na hata shuleni alipenda uongozi na kuanza kuchaguliwa nafasi mbali mbali’’.

Amesema baada ya kugundua uwezo wa kuongoza alionao mtoto wao  walianza kuchukuwa hatua ya kukuza kipaji chake kwa kumsaidia kwa hali na mali mpaka hapa alipofikia.

 "Tulianza kumsaidia kwa kumtiya moyo, kujitahidi kumsomesha  na kwa sasa ili aweze kutekeleza majuku yake ya uongozi vizuri ", alisema mzee Borafya Hamza

Mzee Hamza amewaasa wazazi wenye watoto wenye ulemavu  ambao wana vipaji  kwamba, wasiwalemaze watoto wao badala yake  kuwaunga mkono kwa vipaji walivyonavyo na kuwachanganya kwa watoto weziwao, ili akili zao zitanuke na wajione kama binadamu wengine.

MWANZO WA UONGOZI WAKE MPAKA SASA

 Safari ya Jamila katika uongozi  ilianza rasmi mwaka 2012 ambapo amesema   ‘’nilikuwa waziri wa habari katika serikali ya wanafunzi ya skuli ya Kisiwandui msingi ‘’.

 Amesema baada ya hapo alisitisha kuendeleya na uongozi mpaka alipoingia sekondari ambapo mwaka 2015 alijiunga na club ya TUSEME ndani ya skuli yao Haile Thalasi.

Amesema  mwaka 2016 alingia ndani ya BUNGE LA VIJANA ZANZIBAR baada ya kushida katika uchaguzi na alikuwa ni mjumbe wa kawaida na kuongeza:

 “Mwaka huo huo nikawa mwenyekiti Baraza la Vijana shehia ya Mwanakwerekwe  na baadae kuwa  mjumbe wa kamati tendaji wilaya  ya magharib B Baraza la vijana Zanzibar”

Kwa mujibu wa  Jamila, mwaka 2017  alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa jumuiya ya wasiona Zanzibar katika ngazi ya  wilaya. Mwaka 2018 akawa mwenyekiti  kamati ya vijana michezo katika Baraza la vijana Zanzibar.

“Mwaka, 2018  nilirudi tena Bunge la vijana Zanzibar  na kuchaguliwa Waziri wa Maendeleo ya Vijana Zanzibar’’ amedokeza .

Jamila  amesema  aliingia rasmi kwenye siasa  mwaka 2019  na kuchaguliwa mjumbe wa kamati tekelezaji tawi, ambapo mwaka 2020 aliteuliwa kuwa mjumbe wa kamati ya kupinga vitendo vya udhalilishaji shehia ya Mwanakwerekwe akiwakilisha vijana na watu wenye ulemavu.

Mwaka 2020 pia aligombea uwakilishi katika jimbo la Mwanakwerekwe na mwenyewe anasema ‘’ sikutaka kuanza na viti maluum, lakini katika uchaguzi huo sikufanikiwa kushinda’’.

Hata hivyo amesema  mwaka 2021 alitoka wilaya kwenda taifa Baraza la vijana  kugombania nafasi ya ujumbe baraza la watendaji taifa na akashinda, kwa sasa ndio cheo anachotumikia.

VIONGOZI CHIPUKIZI.

Baadhi ya viongozi chipukizi  wanawake Zanzibar nao wamesema, wanjifunza vitu vingi sanaa kutokana na ujasiri na moyo wa kizalendo alionao Jamila katika uongozi wake.

 Mwajuma Zaidi Makame ni kiongozi chipukizi amesema, "Anajifunza vitu vingi sanaa  kupitia kiongozi Jamila na kwamba ni mfano wa kuigwa na jamii haswa vijana wakike kama sisi ambao ndo kwanza tunachipukia katika uongozi"

Rayyan Makame Abdallah, yeye anasema kwa Jamila ananjifunza  kwamba “Ni muhimu kujitolea kwa wale unaowaongoza”.

Jamila mwenyewe anatoa ushauri kwa vijana wanawake viongozi kwamba, lazima wajiamini wao wenyewe. ‘’Wakijiamini  wao wenyewe wanaweza kufikia malengo yao”

Pia ameshauri kwamba  ili tuweze kufikia lengo la hamsini kwa hamsini lazima vijana waanze kukimbilia fursa mbali mbali katika jamii pindi zinapotokezea. Kujaribu kugombea nafasi za uongozi na amesisitiza vijana kutambua kwamba "kupata na kukosa ni majaliwa lakini utakuwa ushajaribu".  

 WANANCHI WANAOMFAHAMU

Baadhi ya wananchi wanomfahamu Jamila wanasema, ni kijana ambaye ametambua mapema uwezo wake wa kuongoza na anatumia uwezo huo kufikia ndoto zake, na wanaamini atafika mbali sana.

 Juma Bakari Juma anasema "Jamila ni kiongozi kijana mwanamke na ni mlemavu wa macho lakini anajituma sana na namini atakuwa kiongozi mzuri hapo baadae ametambuwa uwezo wake wa kuongoza mapema".

Kwa upande wake Naila Mcha Haji anasema "Jamila ni mfano kwa sisi  vijana wa kike ambao hatuna ulemavu wowote  hapa mtaani kuna kitu cha kujifunza maana Jamila anajituma kama anaona vile".

  

               ‘’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’mwisho’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’’


Post a Comment

1 Comments